Beki Simba aeleza yaliyomkuta kwa Mbeya City

Paul Bukaba

Muktasari:

Beki huyo aliyefungwa bandeji ngumu katika mguu wa kulia, anasema ana matumaini matibabu aliyopata yatamrejesha katika kikosi cha Simba.

Beki wa Simba Paul Bukaba alishindwa kuendelea na mechi iliyopita dhidi ya Mbeya City, baada ya kuumia goti Ijumaa iliyopita.

Baada ya kutolewa uwanjani aliwahishwa hospitali kupatiwa matibabu kutokana na maumivu makali aliyopata.

Bukaba anasema atakuwa nje kwa wiki tatu kabla ya kurejea uwanjani akiwa fiti na matumaini ya kuitumikia Simba katika mashindano ya msimu ujao.

Beki huyo aliyefungwa bandeji ngumu katika mguu wa kulia, anasema ana matumaini matibabu aliyopata yatamrejesha katika kikosi cha Simba.

“Hapa ndio nimemaliza ligi vibaya kwasababu nitakuwa nje ya uwanja wa bila kufanya mazoezi yoyote kwa muda wa wiki tatu, hayo ni matibabu ya awali kwa maana hiyo sitaweza kuwahi kurudi uwanjani mapema msimu huu,” anasema beki huyo wa kati. Mchezaji huyo anasema amepata faraja baada ya kupata ujumbe wa kumfariji kutoka kwa viongozi na mashabiki wa klabu hiyo ambao wamemtakia kila la kheri.

Bukaba atabaki Mbeya na anatarajiwa kurejea jijini na wenzake kesho baada ya kumaliza mchezo wao na Prisons uliochezwa jana kwenye Uwanja wa Sokoine. Awali, Simba ilivuna pointi tatu katika mechi yake dhidi ya Mbeya City walioshinda mabao 2-1.