Chelsea FC ilivyoshikilia rekodi kwa timu za Ujerumani

Chelsea imeendelea kushika rekodi yake katika mashindano ya mbalimbali kwa timu za Ujerumani baada ya kufuzu fainali ya Ligi ya Europa.

Ushindi wa mabao 4-3 iliyopata mwishoni mwa wiki dhidi ya Eintracht Frankfurt katika mchezo wa nusu fainali, umeifanya Chelsea kuendeleza rekodi ya kutofungwa na timu za Ujerumani kwenye uwanja wake wa Stamford Bridge.

Matokeo hayo ni mabaya kwa Frankfurt kwa kuwa imepoteza mechi ya ugenini kwa mara ya kwanza katika michezo tisa. Timu hiyo imeshinda mechi saba katika mashindano msimu huu.

Chelsea imefuzu fainali ya mashindano hayo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2013 iliposhinda mabao 2-1 dhidi ya Benfica ya Ureno timu hiyo ikiwa chini ya kocha wa muda Rafael Benitez.

Pia Chelsea imeingia katika rekodi mpya kwa timu nne za England kukutana zenyewe katika mechi za fainali za Ulaya. Wakati timu hiyo itacheza na Arsenal mechi ya fainali Liverpool itavaana na Tottenham Hotspur kwenye fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Arsenal ilitinga fainali baada ya kuichapa Valencia mabao 4-2 mwishoni mwa wiki. Liverpool ilipata tiketi baada ya kuing’oa Barcelona kwa kuigagadua mabao 4-0.

Wakati timu hizo za England zikiweka rekodi mpya katika ulimwengu wa soka, muuaji wa Chelsea dhidi ya Frankfurt, Edin Hazard, amesema hana uhakika kama mechi ya fainali dhidi ya Arsenal itakuwa ya mwisho.

Hazard ametoa kauli hiyo baada ya kuhojiwa kuhusu mustakabali wake ndani ya klabu hiyo hasa baada ya uvumi kuenea kwamba ana mpango wa kujiunga na Real Madrid katika usajili wa majira ya kiangazi.

“Akilini mwangu bado sijajua hatima yangu,” alisema nahodha huyo wa timu ya Taifa ya Ubelgiji alipokuwa akitoa ufafanuzi.

Mchezaji huyo hakuonyesha ishara ya kuaga mashabiki wa Chelsea baada ya mchezo kumalizika licha ya kufunga penalti ya mwisho iliyoipa ushindi timu hiyo.

Pia matokeo ya Chelsea yanaweza kumuweka kocha Maurizio Sarri sehemu salama msimu ujao baada ya kupata lawama za mashabiki wakidai hana uwezo licha ya kuiongoza timu hiyo kwa msimu mmoja tu.