Mavazi ya Makamu wa Rais yamvutia mchungaji FPCT

Muktasari:

  • Wanawake wengi nchini hivi sasa wanatuhumiwa kuvaa mavazi yanayokwenda kinyume na maadili, hali inayoleta ukakasi kwa watu wengi hasa wanaume.

Kigoma.  Askofu Mkuu wa Kanisa la Free Pentecost Church Tanzania (FPCT), Motomoto Mtamya, amewataka wanawake wa kikristo nchini kuvaa mavazi ya heshima kama ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan aliyesema ni kivutio kwa watu wengi. 

Akizungumza katika Ibada ya kuwekwa wakfu kwa Askofu Mkuu msaidizi na Maaskofu wengine wanne wa kanisa hilo leo Septemba 9, Mchungaji Mtamya amesema wanawake wanatakiwa kuvaa mavazi yanayositiri miili yao kwasababu kwa kufanya hivyo, wataendelea kuwa warembo na watapendeza badala ya kuvaa mavazi ya ovyo.

Amesema mavazi ya makamu huyo wa Rais yanampendeza na kuwa kivutia popote alipo na “Ninyi muigeni yeye kwa kuvaa hivyo.”

Makamu wa Rais huyo amewasili wilayani hapa mkoani Kigoma jana kwa ziara ya kikazi ya siku nne.

Atatembelea miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwamo ya afya, elimu na mazingira kwa kuikagua na baadhi kuiwekea mawe ya msingi.

Leo, Makamu huyo Rais ameshiriki katika ibada ya kuwekwa wakfu kwa maaskofu hao wa kanisa hilo mjini Kigoma.