VIDEO: Mikopo yawaponza wakurugenzi sita Bodi ya Mikopo Elimu ya Juu

Muktasari:

Bodi imewafukuza kazi watumishi hao kwa makosa mbalimbali ikiwamo uzembe

Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imewafukuza kazi wakurugenzi wake sita kwa tuhuma mbalimbali zinazowakabili ikiwamo uzembe kazini.

Akizungumza leo Juni 13, Mkurugenzi wa HESLB Abdul Razac Badru, amesema miongoni mwa tuhuma hizo ni kufanya uzembe na kuisababishia hasara ya mabilioni ya fedha bodi hiyo.

Badru amesema tuhuma nyngine ni kushindwa kutekeleza majukumu yao ya urejeshaji wa mikopo kwa mujibu wa kanuni na taratibu.

Taarifa za kufukuzwa kazi kwa vigogo hao imesainiwa na Mwenyekiti Profesa William Anangisye na imesomwa mbele ya waandishi wa habari leo na Badru.

Waliofukuzwa kazi ni pamoja na mkurugenzi wa urejeshaji mikopo, Hamid Chagonja, mkurugenzi wa upangaji na ugawaji mikopo, Onesmus Laizer na msaidizi wake, John Elias na mkurugenzi msaidizi urejeshaji mikopo, Robert Kibona.

Bodi hiyo imebainisha kuwa imefikia hatua ya kuwafukuza wakurugenzi hao ambao awali walisimamishwa kazi, baada ya kujiridhisha na taarifa ya kamati iliyopewa jukumu la kuwachunguza. 

"Watumishi hao waandamizi walikuwa wanakabiliwa na tuhuma mbalimbali ikiwamo uzembe uliokithiri, hivyo kusababisha hasara na upotevu wa fedha za Serikali, "amesema Badru.

Amesema bodi hiyo imemwagiza kuzitaarifu mamlaka nyingine za Serikali kwa hatua za ziada pale zitakapoona inafaa.

Mwanasheria wa bodi hiyo Abdul Mtibora amesema pamoja na uamuzi huo watu hao wana haki ya kukata rufaa Tume ya Utumishi wa Umma ndani ya siku 45, ikiwa wanaona hawakutendewa haki.