Polisi inawashikilia watu 12 kutekwa kwa bilionea wa Tanzania Mo Dewji

Muktasari:

Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam inawashikilia watu 12 kwa mahojiano ya kutekwa kwa mfanyabiashara Mohamed Dewji ‘Mo’


Dar es salaam. Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema watu wanaoshikiliwa kwa ajili ya kuhojiwa kutokana na tukio la kutekwa kwa mfanyabiashara maarufu nchini Mohamed Dewji ‘MO Dewji’ wamefikia 12.

Mapema leo asubuhi Mambosasa alitaja idadi ya wafanyakazi watatu wa hoteli ya hiyo ndiyo wanashikiliwa kwa mahojiano zaidi.

MO ametekwa alfajiri ya leo Oktoba 11, 2018 katika Hoteli ya Colosseum iliyopo Masaki, jijini Dar es salaam alipokwenda kwa lengo la kufanya mazoezi.

"Kwa sasa wako 12 wakiwamo walinzi wote watano wa Kampuni ya G1 inayosimamia ulinzi wa hoteli hiyo, pia kuna security Manager wa hoteli," amesema Mambosasa alipozungumza na Mwananchi.

Mambosasa amesema hadi sasa hakuna taarifa zozote za awali walizonazo kuhusu kupatikana kwa mwekezaji huyo wa klabu ya Simba mwenye hisa 49.

Soma zaidi: