Reli ya kisasa ya SGR yafikia asilimia 42

Rais John Magufuli akipewa maelezo kuhusu ujenzi wa SRG. Picha ya Maktaba

Fedha kiasi cha Sh2 trilioni zimeshatolewa na Serikali mpaka sasa kwa ajili ya ujenzi wa Reli kwa kiwango cha Kimataifa (SGR) ambao umekamilika kwa asilimia 42.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Ashatu Kijaji juzi alitembelea ujenzi wa Reli hiyo kutoka Dar es Salaam hadi eneo la Soga (kilometa 53) mradi huo na kusema Serikali imedhamiria kukamilisha mradi huo.

Baada ya kukagua shughuli hiyo, Dk Kijaji alieleza kuridhishwa na kasi ya ujenzi na kumpongeza mkandarasi anayejenga reli hiyo, Kampuni ya Yapi Merkezi, kwa kutekeleza jukumu hilo kwa viwango vya hali ya juu.

Naibu Waziri alielezwa kuwa treni ya kwanza kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro inatarajia kuanza safari zake Novemba mwaka huu kama kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa.

Meneja wa mradi wa SGR (Dar es Salaam hadi Morogoro), Mhandisi Machibya Masanja alisema ujenzi wa reli hiyo umekamilika kwa asilimia 42.

“Mradi wetu unaenda vizuri na kwa wakati. Shughuli ya ujenzi na utandikaji reli imeanza Dar es Salaam na inaendelea vizuri. Ujenzi wa daraja umekamilika kwa asilimia 55 na utandikaji wa reli katika jijini utafikia kilometa 10 mwishoni mwa Februari,” alifafanua Masanja.

Reli hiyo inajengwa kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza inatarajia kugharimu zaidi ya Sh7 trilioni, na baadaye itaunganisha mtandao wake na nchi jirani za Congo, Uganda, Burundi na Rwanda.

Katika hatua nyingine, Dk Ashatu Kijaji, alizungumza na wakazi wa eneo la Guluka Kwalala, Gongo la Mboto, wanaotakiwa kulipwa fidia akiwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwaletea maendeleo.

Wakazi hao waliomba Serikali iwasaidie kupata viwanja kwa ajili ya kujenga makazi yao baada ya kulipwa fidia kupisha mradi wa SGR.