Steve Nyerere asema nyama kushikana na mifupa inamtesa

Muktasari:

Msanii wa Bongo Movie, Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ amesema ana wiki mbili yupo kitandani huku akitaja ugonjwa unaomsumbua

Dar es Salaam. Msanii wa Bongo Movie, Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ amesema ana wiki mbili yupo kitandani huku akitaja ugonjwa unaomsumbua kuwa ni nyama kushikana na mifupa.

Steve ambaye alishawahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Bongo Movie, amesema ugonjwa huo umemsababisha kushindwa kufanya kazi yoyote na kushindwa kutembea, huku daktari wake akimshauri apumzike zaidi.

Akizungumzia alichoandaka kwenye ukurasa wake wa Instagram wa kuomba aliyemloga amsamehe, amesema ameandika kama binadamu tu na haoni kama kuna ubaya.

“Unajua katika maisha lazima kuna watu uliwakosea, hivi mimi kuandika vile sioni kama kuna ubaya wowote kikubwa nawaomba Watanzania waniombee niweze kupona na kurudi katika majukumu yangu ya kila siku,”amesema Steve.

Ameeleza tangu aanze kuumwa mahali anapoweza kufika ni kutembea kutoka chumbani hadi sebuleni na sebuleni kurudi chumbani tena kwa kusaidiwa kutokana na maumivu makali anayoyasikia.