Sumaye ataka wanaohama kukemewa

Muktasari:

Sumaye alisema mwanasiasa anayefanya hivyo ni fisadi mkubwa kwani anachezea fedha za wananchi wanazolipa kama kodi.

Dar es Salaam. Waziri mkuu mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Fredrick Sumaye amesema wanajiuzulu ubunge na udiwani kwa kushawishiwa kwa fedha na madaraka wanapaswa kukemewa na watu wote.
Katika mahojiano na kituo cha habari za Azam Two jana Ijumaa Sumaye alisema mwanasiasa anayefanya hivyo ni fisadi mkubwa kwani anachezea fedha za wananchi wanazolipa kama kodi.
"Mtu akijiuzulu kwa sababu za msimamo binafsi hiyo ni sawa lakini akijiuzulu kwa nguvu ya fedha  na madaraka tunapaswa wote kukemea,"alisema Sumaye.
Alihoji uhalali wa mbunge kujiuzulu nafasi hiyo akiwa chama fulani na kuitaka tena nafasi hiyo katika chama kingine kwa madai ya kutaka kuwatumikia wananchi wakati hata huko alikojiuzulu alikuwa na uwezo wa kufanya hivyo.
"Mtu kama ni mbunge na aliwaomba kura wananchi ili kuwatumika  anapaswa kuwatumikia sio kuhama chama na kutaka tena ubunge kwani mbunge kazi yake ni kuwasemea wananchi sio chama chake," amesema Sumaye.