Ukarabati wawavuta walimu kuishi shuleni, wadau waitwa

Muktasari:

  • Sambamba na ukarabati huo, mwalimu Mutungi amesema walimu hao pia wamevutiwa na hatua ya kufungiwa umeme wa jua katika makazi hayo.

Mwalimu mkuu wa Shule ya Msingi Katerero, Denisia Mutungi amesema baada ya nyumba za walimu kukarabatiwa wengi wamevutiwa na mazingira, hivyo kuamua kuishi shuleni.

Sambamba na ukarabati huo, mwalimu Mutungi amesema walimu hao pia wamevutiwa na hatua ya kufungiwa umeme wa jua katika makazi hayo.

Mwalimu huyo ambaye ni miongoni mwa waliokuwa wanaishi mbali na mazingira ya shule alisema hatua hiyo itarahisisha mazingira ya kazi na kufika shuleni mapema tofauti na awali ambapo wengine walichelewa vipindi darasani sababu ya umbali.

Meneja wa kampuni ya Mobisol Kanda ya Ziwa, Nkorwa Nkorangigwa alisema wameamua kuwafungia umeme wa jua katika nyumba sita za walimu hao ili wafurahie kuishi karibu na shule.

Nkorangigwa alisema walimu wanalazimika kupanga mitaani na wengine kutembea umbali wa kilomita 20 kutokana na mazingira ya shule kutokuwa mazuri. Mwenyeki wa Kijiji cha Kanazi ilipo shule hiyo, Haruna Swarehe aliwashauri wadau kuboresha mazingira ya Sekondari ya Bujunangoma ili wanafunzi watakaochaguliwa wasikate tamaa.