Wafugaji waua na kujeruhi Morogoro

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mwigulu Nchemba akiangalia ng'ombe waliokufa wilayani Mvomero.

Muktasari:

Mtu mmoja auawa, wengine watatu wajeruhiwa kwenye mapigano kati ya wakulima na wafugaji kijiji cha Dihimba Turiani

Morogoro.Mkulima mmoja auawa, mwingine ajeruhiwa wakiwemo askari  polisi wawili kwenye mapigano dhidi ya wafugaji wa kimang’ati kwenye kijiji cha Dihimba Turiani, mkoani Morogoro.

 

Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Betty Mkwasa amesema mapigano hayo yametokea baada ya wafugaji kutaka kuwachukua kwa nguvu ng’ombe zaidi ya 150 waliokuwa wakishikiliwa na wakulima kwenye ofisi ya kijiji hicho.

 

Mkwasa amesema siku ya tarehe 11 mwezi huu, mkulima mmoja aliyejulikana kwa jina la Bakari Mulunguza alikuta ng’ombe zaidi ya 150 wakila shambani kwake pasipo kuwa na mchungaji wa ng’ombe hao, ndipo Mulunguza alipoomba msaada kutoka kwa wakulima wenzake kwa pamoja waliwaswaga ng’ombe hao hadi kwenye ofisi ya serikali ya kijiji.

 

Amesema wakulima hao waliamua kuchukua uamuzi huo ili mwenye ng’ombe ajitokeze na kupigwa faini kutokana na uharibifu uliosababishwa na ng’ombe hao. Alisema siku iliyofuata ya tarehe 12, ndipo alipojitokeza mfugaji mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Shaabani Ikeli na kudai kuwa yeye ndiye mmiliki wa ng’ombe hao.

 

“Serikali ya kijiji ilimtaka mfugaji huyo kulipa faini ya Shilingi laki mbili kama fidia kutokana na uharibifu uliosababishwa ; mfugaji huyo alikubali na kuahidi kuwa angelipa faini hiyo, lakini cha kushangaza alirudi na kundi kubwa la vijana wafugaji wakitaka kuwachukua ng’ombe kwa nguvu, ndipo mapigano yalipotokea,” alisema Mkwasa.

Alimtaja aliyeuawa kuwa ni Mohamed Musa (43) mkulima wa kitongoji cha Kaole, na aliyejeruhiwa ni Charles Paulo (35) ambaye amelezwa hospitali ya Bwagala Turiani kwa matibabu.

Mkwasa amesema kitendo hicho kiliamsha hasira kwa wakulima ambao walilipa kisasi kwa kuwakatakata miguu na sehemu mbalimbali za miili ng’ombe 150. Alisema polisi walifika eneo la tukio na kudhibiti vurugu hizo; amesema polisi wawili wamejeruhiwa kweye mapigano hayo.