Waziri Lukuvi aagiza kufukuzwa kazi Ofisa Ardhi Monduli

Waziri wa Ardhi, nyumba na maendeleo ya Makazi William Lukuvi

Muktasari:

  • Waziri Lukuvi amemsimamisha kazi Ofisa Ardhi  Wilaya ya Monduli, Kitundu Mkumbo kwa kumilikisha ardhi zaidi ya hekari 1500 kinyume cha sheria.

Monduli. Waziri wa Ardhi, nyumba na maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameagiza kufukuzwa kazi Ofisa Ardhi wa wilaya ya Monduli Kitundu Mkumbo kwa kukiuka sheria na taratibu za utoaji wa hati miliki za kimila.

 Waziri Lukuvi ametoa agizo hilo leo Septemba 12 mbele ya wakazi wa kijiji cha Engarooji wilayani Monduli mkoani Arusha ambao wamekua katika mgogoro wa ardhi kwa muda mrefu.

 Mgogoro huo umechangia   wakazi hao kugawanyika katika makundi mawili yasiyoelewana.

 Akizungumza leo, Waziri Lukuvi amefafanua kuwa mwenye mamlaka ya kumilikisha mtu ardhi zaidi ya hekari 50 ni Rais pekee.

 "Ofisa huyu wa ardhi ambaye japo hapo awali mlishawahi kumsimamisha kazi kwa makosa mengine kama haya, lakini  kwa sasa makosa haya ni makubwa sana na sasa afukuzwe kazi, haiwezekani amilikishe hekari zaidi ya  hekari 1,500 kinyume na sheria," amesema Lukuvi.

 Katika hatua nyingine Waziri Lukuvi amezifuta hati zote za kimila zilizotolewa na Ofisa Ardhi huyo kwa sababu zimetolewa kinyume na utaratibu kwa mujibu wa sheria ya ardhi ya mwaka 1999 ambayo hairuhusu kutoa hatimiliki za kimila zaidi ya hekari 50 bila idhini ya Rais.

 Miongoni mwa waliomilikishwa maeneo makubwa katika kijiji cha Engarooji wilayani Monduli ni Paulo Ndari mwenye hekari 716, Lekashu Ng’ene mwenye hekari 301 na Salimu Orkoskos mwenye hekari 268 ambazo zote pamoja na nyingine Waziri Lukuvi amezifuta.