Polisi waipokonya bendi vifaa ilivyopewa na Kayihura

Jenerali Kale Kayihura

Muktasari:

Polisi mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa vile si msemaji alisema vifaa hivyo vya muziki vilipelekwa kwenye bendi hiyo enzi za uongozi wa Jenerali Kayihura

Kampala, Uganda. Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Martins Okoth-Ochola ametoa maagizo ya kuipokonya bendi ya Nyakabande Town vifaa vya muziki ambavyo ilipewa enzi za uongozi wa Jenerali Kale Kayihura kwa maelezo kwamba iligawiwa kimakosa.
Baada ya kutolewa maagizo hayo, maofisa polisi kutoka kitengo cha PSU waliivamia bendi hiyo ya wilayani Kisoro mwishoni mwa wiki iliyopita na kupokonya vifaa husika. Vifaa hivyo bado vilikuwa na nembo ya polisi.
Polisi mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa vile si msemaji alisema vifaa hivyo vya muziki vilipelekwa kwenye bendi hiyo na maofisa waandamizi enzi za uongozi wa Jenerali Kayihura bila kufuata taratibu zilizowekwa.
Polisi huyo alisema mameneja wa bendi ya polisi walipinga kuondolewa kwa vifaa hivyo bila kufuata taratibu lakini hawakufungua malalamiko yoyote hadi alipoteuliwa Ochola kushika nafasi hiyo.
Mwaka jana, bendi hiyo ilimwomba Jenerali Kayihura, ambaye alikuwa IGP wakati huo kuangalia uwezekano wa kupata vifaa vipya vya muziki na aliahidi kuwasaidia.