Mzumbe Dar es salaam yapewa cheti cha ubora mafunzo ya uhasibu wa juu

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji akimkabidhi cheti cha kituo bora cha mafunzo Mkuu wa Kampasi ya Dar es salaam ya Chuo Kikuu Mzumbe Prof. Honest Ngowi katika mahafali ya 41 ya Bodi ya Taifa ya Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA) yaliyofanyika October 5,2019 jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Kwa mara ya pili mfululizo Chuo Kuu cha Mzumbe tawi la Dar es Salaam kimetambulika kuwa kituo bora cha mafunzo ya uhasibu na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA).

Chuo hicho kimepokea tuzo hiyo wakati wa mahafali ya 41 ya wahasibu ambapo wanafunzi walitunukiwa vyeti vya ngazi mbalimbali zinaotambulika na NBAA.

Mkuu wa chuo hicho, Profesa Honest Ngowi amesema ni mara ya pili kupokea tuzo hiyo yenye maana kubwa katika kukuza taaluma ya uhasibu nchini.

“Tumepata tuzo hii kwa sababu ya kuwa na walimu bora wenye uzoefu wa kufundisha uhasibu. Vilevile tuna maktaba nzuri na miundombinu bora ya kusomea mbayo inakidhi mahitaji ya wanafunzi hivyo tuzo hii inatufanya tuendelee koboresha zaidi hasa upande wa teknolojia kwani uhasibu sasa unabadilika kila siku,” amesema Profesa Ngowi.

Wenyekiti wa bodi ya NBAA, Profesa Isaya Jairo amesema idadi ya wahitimu wa CPA iliongezeka na kufika 817 kutoka 516 wa mwaka jana.

Profesa Jairo alitumia fursa hiyo kuwashauri wahitimu kufahamu majukumu yao na kusaidia kuvutia wawekezaji.