Watalii 340 kutoka China ni kama tone la maji baharini

Dar es Salaam. Balozi wa Tanzania nchini China, Mbelwa Kairuki amesema watalii 343 waliopokelewa hivi karibuni kutoka Taifa hilo la Asia ni kama tone la maji baharini.

Kairuki amesema hayo alipozungumza na gazeti hili kutaka kujua muendelezo wa hamasa hiyo kuwaleta watalii wengi zaidi kutoka China.

“Tulichofanya ni kupanda mbegu. Kundi lililokuja ni la waandishi, wafanyabiashara na wasanii ambao tunatarajia watasaidia kututangaza kwenye vyomvo vyao vya habari na mitandao ya kijamii ili Wachina wengi zaidi wavutike. Lakini hatupaswi kuridhika au kubweteka. Mbegu tuliyopanda lazima tuipalilie, tunyunyizie dawa, tung’oe magugu hadi mbegu ichipuke na tuvune matunda,” amesema Kairuki.

Endapo hayo yatafanywa kimkakati, amesema italipa baada ya miaka mitano ijayo na kuendelea kwa kuwa soko la utalii la China lenye zaidi ya watu milioni 120 wanaokwenda nje kila mwaka, ni la uhakika.

“Tukiweza kujitangaza tukaongeza idadi ya wanaokuja kutoka 34,000 wa sasa hadi 50,000 kwa mwaka ifikapo mwaka 2021 na 100,000 mwaka 2025, tutakuwa mahala pazuri kuwaza idadi kubwa zaidi mfano watalii 500,000 mpaka milioni moja kwa mwaka baada ya miaka 15 hadi 20 ijayo,” amebainisha Kairuki.

Watalii hao kutoka China wameingia nchini siku chache baada ya wageni wengine zaidi ya 1,000 kutoka Islael kutembelea vivutio vilivyopo nchini.

Watalii hao kutoka China waliopokelewa na viongozi kadhaa wa Serikali walioongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa pamoja na menejimenti ya Benki ya NMB ambao ndio wadhamini wa ugeni huo.

Waziri mkuu aliipongeza kampuni ya Tash-road International Group kwa kuingia makubaliano ya kuwaleta watalii Tanzania ambao ni mwanzo mzuri wa kujitanua na kuutangaza utalii katika anga za kimataifa.

Meneja wa NMB anayeshughulikia dawati la China, Agness Mulolele alisema NMB inaunga mkono jitihada za kukuza utalii hivyo imesogeza huduma karibu ili kuwahudumia wageni wanaoingia nchini.

“Mkoa na wilaya yoyote watakayoenda, sisi tupo na tutawahudumia,” alisema Agness.