Bashe ashauri utengenezwe mpango kabambe sekta ya ufugaji

Mbunge wa Nzega Mjini (CCM) Hussein Bashe akichangia mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mifungo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2019/2020 bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

  • Mbunge wa Nzega (CCM) Hussein Bashe ameshauri mambo mbalimbali kuboresha sekta ya ufugaji Tanzania ikiwemo kuandaa mpango utakaoshirikisha wizara nyingine.

Dodoma. Mbunge wa Nzega (CCM) Hussein Bashe amesema suala la ufugaji ni mtambuka na hivyo kushauri Wizara ya Mifugo na Uvuvi itengeneze mpango kabambe utakaoshirikisha wizara nyingine

Bashe ameyasema hayo leo Mei 22, 2019, wakati akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa mwaka 2019/2020.

Amesema suala la viwanda litakiwa ni  kuhakikisha kuwa mali ghafi ya maziwa inapatikana ili mzalishaji aweze kuyapata na kuyanunua.

Bashe ametoa hesabu ya kulisha ng’ombe mmoja kitaalam kuwa ni Sh5,000 kwa siku na kwamba wastani wa ng’ombe wengi wanatoa maziwa lita 10 kwa siku na wachache lita 30.

Amesema wastani wa bei ya maziwa ni kati ya Sh900 hadi 1,000 kwa lita na kumfanya mzalishaji wa lita 10 kupata Sh9,000.

Amesema kwa kugharamia mahitaji mengine ya ufugaji, mfugaji hapati faida yoyote kwa ufugaji na hivyo kuamua kufuga kawaida.

“Mfugaji hawezi kuzalisha vizuri. Waje na Master Plan, washirikishe wizara nyingine. Ni suala mtambuka si la Mpina pekee,” amesema.

Bashe amepongeza uamuzi wa Serikali kutotoa kibali kwa Tanga Fresh cha kuagiza maziwa toka nchini Rwanda.

Amesema walichofanya Rwanda ni kuwapatia kila kaya ng’ombe mmoja na kutengeneza vituo vya kukusanyana maziwa katika maeneo mbalimbali.