Benki ya NMB yatoa Sh9.5 bilioni kwa wakulima 2997

Dar es Salaam. Benki ya NMB imetoa Sh9.5 bilioni za mkopo kwa wakulima 2,997 wa korosho wa Mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Pwani kwa ajili ya kununua  pembejeo.

Lengo ni kuwajengea uwezo wakulima na kuiongezea  thamani sekta ya kilimo ambayo ni tegemezi kwa uchumi wa Taifa.

Hayo yameelezwa na kaimu mkurugenzi mtendaji wa NMB, Filbert Mponzi katika hafla ya kuingia ubia na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB).

Amesema  benki hiyo  inatambua umuhimu wa sekta ya kilimo katika uchumi, na ndiyo maana imeona  haja ya kuwawezesha wakulima.

“Ubia tulioingia naTADB una lengo la kufanikisha msimu wa korosho wa mwaka 2019/20. Wakulima wanahitaji fedha za pembejeo kwa ajili ya msimu mpya,  tunafanya kila linalowezekana kuunga mkono juhudi za Serikali za kuendeleza sekta ya kilimo."

“Kwenye korosho wote tunafahamu changamoto zilizojitokeza msimu uliopita,  kuna wakulima bado hawana fedha za pembejeo, tumeona tulipatie ufumbuzi hilo kwa kushirikiana na wenzetu wa TADB,” amesema.

Naibu Waziri wa Kilimo,  Hussen Bashe amepongeza jitihada zinazofanywa na benki hiyo na  kuziomba taasisi nyingine za fedha kuongeza mikopo kwenye kilimo.

Amesema mikopo hiyo ni chachu katika kuinua  uwekezaji kwenye sekta hiyo inayochangia asilimia 25 hadi 30 ya pato la Taifa.

“Niziombe taasisi za fedha ziendelee kupunguza riba angalau mwaka kesho ifike asilimia 15 na tutashukuru zaidi kama itashuka zaidi hadi 12 au 10 hapo tutasaidia kuinua uwekezaji kwenye sekta ya kilimo.

“Upande wetu  kama wizara tunaendela kuzipitia sera zetu ili kuzifanya taasisi hizi kuwa na uhakika zinapopeleka fedha kwenye kilimo na kuwezesha uwekezaji kufanyika,” amesema Bashe