CRDB kuongeza uwekezaji huduma za kidigitali

Mkurugenzi mtendaji wa benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela,

Muktasari:

Wanahisa wa Benki ya CRDB wanakutana jijini Arusha katika mkutano wa mwaka wa 24 ambao umetanguliwa na semina kwa wanahisa.

Arusha. Benki ya CRDB imejipanga kuendelea kuwekeza zaidi katika huduma za kidigitali ili kutoa huduma bora zaidi kwa wateja wake.

Mkurugenzi mtendaji wa benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, alitoa taarifa hiyo leo katika semina ya wanahisa wa benki hiyo.

Nsekela amesema benki hiyo licha ya kuwa na matawi 263 na wakala zaidi ya 800 inaamini kuwa kwa kuboresha uwekezaji kidigitali watawafikia wateja wengi zaidi.

Amesema mkakati wao ni kuendelea kutoa huduma bora lakini pia kusaidia kukuza uchumi wa nchi.

Hata hivyo, amesema benki hiyo inaendelea kufanya vizuri na kuongoza kati ya benki zote kwa kupata faida kubwa.

“Lakini pia gawio la benki kwa Serikali limeongezeka na mwaka jana tumetoa kiasi cha Sh19.5 bilioni," amesema.

Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi wa benki hiyo, Ally Hussein Laay amesema Watanzania wengi hawana mwamko katika masuala ya hisa na soko la hisa na kutaka kuwepo mitaala ya masuala ya hisa mashuleni.

Amesema katika soko la hisa la Dar es salaam kwa wastani, hisa 1.7 milioni huuzwa kwa siku zikiwa na thamani ya Sh460 milioni wakati nchi jirani ya Kenya, kwa siku hisa 19 milioni huuzwa na kuingiza  zaidi ya Sh10 bilioni.

"Watanzania wengi bado hawawekezi katika hisa na badala yake wamekuwa wakiwekeza katika  kununua nyumba, magari na vitu vingine," amesema.