Mkazi wa Zanzibar aibuka mshinda wa chemsha Bongo ya Tigo

Mtaalam wa Huduma za ziada-Tigo, Fabian Felician na  Jehud Ngolo- Afisa Mwandamizi Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania. wakimpigia simu Shaban Khamis Ali,mkaazi wa Zanzibar, mshindi wa promosheni ya Tigo Chemsha bongo.

Dar es Salaam. Mkazi wa Zanzibar Shabani Khamis Ali (48) leo ameibuka mshindi wa Droo ya mwisho ya ‘Tigo Chemsha Bongo’ imefanyika jijini Dar es Salaam na kujinyakulia gari mpya aina ya Renault KWID yenye thamani ya Sh23m.

Khamis akiongea baada ya  kutangazwa kuwa ameibuka mshindi, alisema anayo furaha kufanikiwa kuwa miongoni mwa washindi wa shindano hilo na kujishindia gari mpya.

“Sikutegemea kabisa kuwa ningeibuka mshindi katika promosheni hii, habari hizi naziona kama ndoto kwangu, nashukuru Tigo kwa kunifungia mwaka vizuri na kutimiza ndoto yangu ya kumiliki gari, kwani itanisaidia katika mizunguko yangu, “alisema kwa Khamis.

Mtaalam wa Huduma za Ziada kutoka Tigo, Fabian Felician, alimpongeza mshindi huyo na kutumia fursa hiyo kuwashukuru wateja wote walioshiriki na baadhi yao kujishindia zawadi mbalimbali ikiwemo zawadi za fedha taslimu.

“Tunayo furaha kubwa katika kipindi hiki cha kuelekea katika msimu wa sikukuu kumpata mshindi wetu wa gari ya aina Renault Kwid,yenye thamani ya 23m/-, gari hili ni jipya kabisa, baada ya kumpata mshindi taratibu zengine zitafata ili tuweze kumkabidhi Shaban Khamis Ali gari lake jipya,” alisema Felician.

Aliongeza kuwa, promosheni hii ambayo ilianza jijini Mwanza katika msimu wa Tigo Fiesta 2019-Saizi Yako  imepata mafanikio makubwa kutokana na wateja wengi kujitokeza kushiriki na baadhi yao kufanikiwa kujishindia fedha taslim na hivyo Tigo kufanikisha lengo lake ambalo lilikuwa ni kuwashukuru wateja kwa kuiunga mkono kampuni kupitia kununua bidhaa zake mbalimbali.

Kwa kumalizia Felician aliwashukuru wateja wote wa Tigo kwa kuendelea kuunga mkono kampuni na kuahidi kuwa promosheni mbalimbali za kunufaisha wateja wa kampuni hiyo zinatendelea kubuniwa katika siku za usoni.