Mviwata: Serikali isitishe viini tete

Mwenyekiti wa Mviwata Taifa, Veronica Sophu

Muktasari:

Wakizungumza katika mdahalo wa sera za sekta kilimo mjini Morogoro mwishoni mwa wiki iliyopita, walisema mbegu za viini tete zimekuwa na madhara kwa wakulima na kupoteza uasili wa mbegu.

Morogoro. Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Wadogo Tanzania (Mviwata), umeitaka Serikali kusitisha matumizi ya mbegu za viini tete kwa madai kuwa hazina manufaa kwa wakulima.

Wakizungumza katika mdahalo wa sera za sekta kilimo mjini Morogoro mwishoni mwa wiki iliyopita, walisema mbegu za viini tete zimekuwa na madhara kwa wakulima na kupoteza uasili wa mbegu.

Mwenyekiti wa Mviwata Taifa, Veronica Sophu alisema Serikali isiporuhusu uingizwaji wa mbegu za viini tete nchini, wakulima hawatanufaika na mazao yao kwani kwa sasa yanapoteza ubora wake.

Alisema ni vema Serikali ikasimamia sheria na sera za mbegu zenye kuwanufaisha wakulima na kutokubali kuhadaiwa na kampuni za nje zinazotafuta masoko baada ya kukataliwa katika nchi za Ulaya.

Mkuu wa Idara ya Uchumi, Kilimo na Biashara kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Profesa Damian Gabagambi alisema tatizo lililopo ni wakulima wadogo kutoshirikishwa na kusababisha kukithiri kwa migogoro ya wakulima na wafugaji.