Ole wenu mnaokwepa kulipa kodi - TRA

Richard Kayombo.

Muktasari:

Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), imesema haitatishika wala kuyumbishwa na mfanyabiashara yeyote kutekeleza majukumu yake kutokana na nguvu iliyoongezewa na Rais John Magufuli.

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), imesema haitatishika wala kuyumbishwa na mfanyabiashara yeyote kutekeleza majukumu yake kutokana na nguvu iliyoongezewa na Rais John Magufuli.

Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Huduma kwa Walipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo alitoa kauli hiyo jana, alipokuwa akifafanua kuhusu operesheni ya maofisa wa TRA katika bandari kavu zote kwa lengo la kuhakikisha hakuna mianya ya ukwepaji kodi.

Jana saa 7:00 mchana waandishi wa gazeti hili walipata taarifa za maofisa wa TRA walioingia katika Bandari Kavu ya Bollore African Logistics, iliyopo Tabata Relini kwa ajili ya ukaguzi wa mizigo, lakini baada ya kufika ofisi hizo hawakupata ushirikiano wa taarifa za ukaguzi huo.Mmoja wa maofisa wa bandari hiyo, Jane Salala alisema hawezi kutoa ushirikiano kwa kuwa hana mamlaka ya kuzungumzia suala hilo, badala yake alitaka atafutwe msemaji ambaye hakupatikana.