VIDEO: Serikali ya Tanzania yapunguza bei mbolea ya Urea

Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo kuhusiana na Mbolea. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Waziri wa Kilimo nchini Tanzania, Japhet Hasunga amesema kuanzia kesho Alhamisi Februari 20, 2020 mbolea ya Urea itauzwa Sh51,700 kwa mfuko wa kilo 50 badala ya Sh54,000 ya awali.

Dar es Salaam. Waziri wa Kilimo nchini Tanzania, Japhet Hasunga amesema kuanzia kesho Alhamisi Februari 20, 2020 mbolea ya Urea itauzwa Sh51,700 kwa mfuko wa kilo 50 badala ya Sh54,000 ya awali.

Hasunga ametangaza bei hizo leo Jumatano Februari 19, 2020 katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa uagizaji wa mbolea na namna Serikali ilivyojipanga kuhakikisha wakulima wanaipata kwa wakati.

“Najua wengi watasema wengine wameshanunua, lazima bei ipungue. Kwa wastani bei ya rejareja ya Urea ilikuwa Sh54,000 lakini sasa hivi bei mpya ni Sh51,700 kwa wastani, utaona bei imepungua kwa Sh2,300.”

“Punguzo hili litakuwa chachu ya kuwavutia  wakuliwa na wadau mbalimbali na litaanza kutumika kuanzia Februari 20, 2020” amesema Hasunga.

Hasunga amesema kwa Dar es Salaam, bei elekezi  ya awali ilikuwa Sh45,280 sasa hivi bei mpya itakuwa 43,100  lakini kampuni zina uwezo wa kuuza chini ya bei hiyo na sio kuzidisha.

Amesema Arusha bei  ya mbolea hiyo itakuwa Sh51,354 kutoka Sh53,726 ya awali, Dodoma Sh49,923 kutoka 52,296,  Mbeya Sh 52,290 kutoka Sh54,663 na Morogoro Sh49,026  kutoka Sh51,398.

“Mkoa wa Rukwa itauzwa Sh56,000 kutoka Sh58,378 na Tanga itakuwa Sh49,021  kutoka 51,393,” amesema Hasunga.

Amesema wadau, wauzaji, mawakala na yeyote anayehusika na mbolea anatakiwa kuzingatia bei hizo mpya zilizotolewa na Serikali, akisema lengo ni kuhakikisha upatikanaji huduma unakuwa wa kuridhisha.