Tofauti ya matumizi ya simu baina ya wanawake na wanaume inavyozidi kupungua

Taasisi ya Gate (The Gates Foundation) imewashauri mawaziri wa fedha kutoka katika nchi zinazounda kundi za G7 kuunga mkono mkakati wake wa kuondoa utofauti wa matumizi ya huduma za kidijitali kati ya wanaume na wanawake barani Afrika.

Akizungumza hivi karibuni juu ya mkakati huo, mke wa bilionea Bill Gates, Melinda Gates alisema ni lazima kuhakikisha tofauti hiyo inapungua au kuondoka kabisa kwani kuna hatari huduma za teknolojia ya kidijitali na huduma za kifedha kwenye simu zikawapita wanawake wengi barani Afrika, kitu kitakachosababisha kuwa kikwazo cha kuwainua wanawake.

Alisema si Tanzania pekee yenye tofauti bali hata kwa maeneo mengine barani Afrika kuna utofauti kubwa ya matumizi ya huduma za kidijitali kati ya wanaume na wanawake.

Takwimu zinaonyesha kuwa kwa upande wa Tanzania, utofauti katika umiliki wa simu kati ya makundi hayo mawili ni asilimi 9, huku ule wa matumizi ya intaneti kupitia simu ikiwa ni asilimia 41.

Melinda Gates aliipongeza Tanzania kuwa kuna jambo jema linaendelea kuondoa changamoto hiyo kwani makampuni binafsi ya simu yalipo Tanzania yanafanya na kuanzisha mikakati ya kuhakikisha utofauti huo unapungua au kuondoka kabisa.

Alitolea mfano kampuni ya Tigo Tanzania kuwa imechukua hatua madhubuti kuhakikisha huduma ya fedha kwenye simu inapatika nchi nzima kupitia huduma yake ya Tigo Pesa.

 

Alisema Tigo Pesa imebuniwa katika mfumo ambao unahakikisha kuwa unaweza kutimiza mahitaji yote ya wateja mbali na kutoa huduma ya mawasiliano pia inatoa huduma zingine nyingi kama vile mikopo midogo, huduma za kuhifadhi fedha, na bima. Hivi karibuni Tigo imetoa msaada wa mamia ya simu kwa wanawake na wasichana ili kuhakikisha wanaweza kupata huduma za kifedha kupitia simu zao na kufanya matumizi yao, lengo ni kuwawezesha wanawake katika masuala ya kidigitali.

Huduma za kibenki kupitia simu zimekuza uchumi wa watu wengi barani Afrika. Kwa upande wa Tanzania peke yake, idadi ya watu ambao hawajajumuishwa kwenye masuala ya kifedha imepungua kati ya 2009 na 2017. Mafanikio hayo kwa kiasi kikubwa yanahusishwa na kukua kwa huduma za kifedha za kidijitali, zaidi huduma za kifedha kupitia simu.

Kampuni ya ushauri, McKinsey hivi karibuni ilikadiria kuwa ifikapo mwaka 2025 huduma za kifedha za kidijitali zitawasaidia takribani watu bilioni 1.6 duniani kote kuingia katika uchumi rasmi.

Kampuni binafsi kama Tigo kwa upande wa Tanzania imeonesha njia katika kuhakikisha kunakuwa na ushiriki mkubwa katika masuala ya kifedha hasa kwa upande wa wanawake.

McKinsey ilisema Kwa upande wa Kusini mwa Jangwa la Sahara, uwezekano wa wanawake kutokumiliki simu ni asilimia 13, huku uwezekano wa wao kutotumia huduma za intaneti ikilinganishwa na wanaume ni asilimia 41.Jambo hili limekuwa na athari hasi kwa wanawake hasa linapokuja suala la kujitegemea kiuchumi.