Wakulima wa mboga walia, soko hakuna!

Muktasari:

  • Akizungumza kwa niaba ya wanakikundi cha mbogamboga wilayani hapa jana, Nice John alisema wanalima mboga hizo bila kuwa na soko la uhakika hali inayowafanya kupata hasara ikilinganishwa na gharama za uzalishaji.

Hai. Wakulima wa mbogamboga wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, wameiomba Serikali kuwapatia masoko ya uhakika na maeneo ya kutosha kwa ajili ya kilimo hicho.

Akizungumza kwa niaba ya wanakikundi cha mbogamboga wilayani hapa jana, Nice John alisema wanalima mboga hizo bila kuwa na soko la uhakika hali inayowafanya kupata hasara ikilinganishwa na gharama za uzalishaji.

John alisema iwapo Serikali itawasaidia kupata soko la uhakika na maeneo ya kutosha kwa ajili ya kilimo hicho, itawasaidia kujikwamua na umaskini.

Naye meneja wa mradi wa kuwawezesha wanawake kiuchumi mkoani Kilimanjaro kupitia shirika linalolinda na kutetea haki za Wanawake (Kwieco), Stewart Nathaniel alisema wameanzisha mradi huo kuwasaidia wanawake baada ya kuona wengi wao wananyanyasika katika familia.

Nathaniel alisema kwamba baada ya kuona fursa ya kuwapo kwa watalii wengi mkoani hapa waliwahamasisha wanawake hao kwa kuwatafutia wataalamu wa kilimo hasa cha mbogamboga.