Wakulima wahaha na mihogo kichwani

Muktasari:

Tayari China imetangaza kujenga kiwanda cha kusindika muhogo wilayani Handeni, Tanga

Kibondo. Wakati wakulima maeneo ya Pwani wakihamasishwa kulima zaidi mihogo kutokana na kuwa na soko kubwa nchini China, hali ni tofauti kwa wakulima wa zao hilo wilayani hapa ambao wanalazimika kwenda nchi za Burundi na Rwanda kusaka soko.

Wakitoa malalamiko yao mbele ya naibu waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditiye aliyekuwa ziarani wilayani hapa juzi, wakazi hao walisema bei ya zao hilo nchini imeshuka kutoka Sh600 mwaka jana na hadi Sh120 mwaka huu.

Mkulima Mustafa Buchuro aliwatupia lawama madalali ambao wamechangia kwa namna moja au nyingine kushuka kwa soko hilo.

“Madalali hawa wanawafuata wakulima shambani na kupanga bei wenyewe hali hii inachangia kwa kiwango kikubwa kushuka kwa soko,” alisema.

Hata hivyo, ofisa biashara na masoko wa wilaya hiyo, Matiko Masumbuko alipiga marufuku madalali kujihusisha na ununuzi wa mihogo kwa wakulima huku akionya atakayekamatwa atachukuliwa hatua kali za kisheria.

“Kuanzia sasa hakuna mkulima kufuatwa shambani lakini nyie wakulima mnatakiwa kujihurumia wenyewe, muwe na ushirikiano wa kudhibiti hao madalali na muwe na mipango ya pamoja kuhusu bei hali itakayokomesha hasara hiyo,” alisema Masumbuko.

Akizungumzia suala hilo, Nditiye aliagiza wakulima kuanza utaratibu wa kupeleka zao hilo ghalani na biashara ifanyikie huko na si shambani.

Nditiye alisema wamefanya mazungumzo na mashirika ya dini na la chakula duniani (WFP) kwa ajili ya kununua zao hilo, hivyo ni vyema wataifuata ghalani na si nyumbani au shambani.

“Tutauza kwa bei elekezi ambayo haitamuumiza na kumsababishia mkulima hasara,” alisema Ndintiye.