Bibi wa miaka 106 apona corona Uingereza

Muktasari:

Bibi mwenye umri wa miaka 106 nchini Uingereza, Connie Titchen  amepona ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya corona na ameruhusiwa kutoka hospitali.

Dar es Salaam. Bibi mwenye umri wa miaka 106 nchini Uingereza, Connie Titchen  amepona ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya corona na ameruhusiwa kutoka hospitali.

Bibi huyo anatajwa kama mgonjwa mzee kuliko wote aliyepona ugonjwa huo uliosababisha vifo vya watu zaidi ya  130,000 duniani.

Machi 26, 2020 bibi mwenye umri wa miaka 102 alipona corona nchini Italia  baada ya kukaa hospitali kwa siku zaidi ya 20.

Connie alipigiwa makofi na wahudumu wa hospitali ya Birmingham's City Jumanne ya Aprili 14, 2020 baada ya kulazwa katika hospitali hiyo kwa wiki tatu.

Bibi huyo aliyekuwa akifanya kazi ya kuuza duka alilazwa katikati ya mwezi Machi 2020 akidaiwa kuwa na ugonjwa pneumonia, hospitali hiyo ilieleza.

Baada ya kuruhusiwa alisema anajisikia mwenye bahati kuvishinda virusi vya corona na ana shauku kubwa ya kuiona familia yake.

Mjukuu wa Bibi huyo, Alex Jones amesema kuwa bibi yake ni mtu anayependa kujishughulisha, kucheza, kuendesha baiskeli na kucheza gofu.

Jones amesema bibi yake amekuwa anapenda kupika chakula chake mwenyewe.

Amebainisha kuwa siri ya bibi huyo kuwa na umri huo akiwa na nguvu ni kwa sababu anapenda kujishughulisha na kuwa huru kufanya mambo yake mwenyewe.