Kijana mbaroni kwa kuiba simu ya askari wa zamu kituoni

Kampala. Polisi wilayani Iganga nchini Uganda wanamshikilia kijana mwenye umri wa miaka 22 kwa tuhuma za kuiba simu ya askari wa zamu katika kituo hicho.

 Mtuhumiwa ambaye ni mkazi wa Jinja, aliingia katika kituo hicho jana Alhamisi akijifanya ni mlalamikaji aliyekwenda kuripoti tukio la wizi, badala yake akaiba simu ya askari aina Tecno.

Gazeti la The Daily Monitor limemnukuu Mkuu wa Polisi wilayani humo, David Ndaula akisema askari huyo alishutuka alipoona simu yake iliyokuwa kaunta haionekani na kumshuku mtuhumiwa, ndipo akaamua kumsachi na kukuta jamaa kashaitia mfukoni.

Baada ya kumtia mbaroni,  polisi walikwenda kusachi nyumbani kwake na kukuta kompyuta mpakato kadhaa na simu nyingine nyingi, zote zikidhaniwa ni zimeibwa katika maeneo mbalimbali.

Kamanda  huyo alisema mtuhumiwa anashikiliwa katika Kituo cha polisi Iganga akisaidia upelelezi.