Ndege yaanguka na kuua 18 DRC

Takriban abiria 16 na wafanyakazi wawili wa ndege wanaaminika kufariki baada ya ndege waliyokuwa wakisafiria kuangukia katika mji wa Goma,  mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Gavana wa Jimbo la Kivu Kaskazini, Nzanzu Carly amesema kuna watu wamefariki katika ajali hiyo lakini hakutoa idadi kamili.

Ndege hiyo ilianguka juu ya nyumba katika eneo jirani la Mapendo baada ya kushindwa kupaa katika uwanja wa ndege wa mji huo, alisema akinukuliwa na CCM.

Wakazi wa eneo hilo ni miongoni mwa waathiriwa wa ajali hiyo, kulingana na vyombo vya habari vya eneo hilo.

Ndege hiyo aina ya Doenier 228 ilikuwa ikimilikiwa na kampuni binafsi ya Busy Bee. Ilitarajiwa kuelekea Beni, umbali wa kilomita 350 kutoka kaskazini mwa Goma wakati ilipoanguka dakika moja baada ya kupaa.

Ajali za ndege hutokea mara kwa mara nchini DRC kutokana na viwango vya chini vya usalama na kutorekebishwa kwa ndege hizo.

Ndege zote za kibiashara za taifa hilo zimepigwa marufuku kufanya biashara katika Muungano wa Ulaya.