Shambulizi la waasi laua askari 89 wa jeshi la Niger

Muktasari:

  • Askari 89 wa jeshi la Niger wanadaiwa kuuawa katika shambulizi la waasi lililofanyika Alhamisi katika mji wa Chinagodrar uliopo Magharibi mwa Niger. Hata hivyo, inahofiwa idadi ya vifo hivyo itakuwa zaidi ya 89.

Niger. Idadi ya vifo vya wanajeshi katika shambulizi la Alhamisi lililotekelezwa na waasi katika kambi ya jeshi la Niger imeongezeka mpaka kufikia watu 89, shambulizi hilo likiwa kubwa zaidi likilinganishwa na lililofanyika mwezi uliopita ambalo liliua askari 71.

Katika taarifa za awali, serikali ya Niger ilisema wanajeshi 25 waliuawa kwenye shambulizi hilo ambalo lilitekelezwa katika mji wa Chinagodrar uliopo Magharibi mwa nchi hiyo na wauaji waliokuwa wamepanda pikipiki na magari.

Vyanzo vinne vya habari vililieleza shirika la habari la Reuters kwamba askari 89 wa jeshi la Niger waliuawa kwenye shambulizi hilo na kuzikwa jana katika Makao Makuu ya Taifa hilo, Niamey.

Chanzo kimoja kilieleza kwamba idadi ya vifo inaweza kuwa zaidi kwa sababu askari wengine walizikwa haraka Alhamisi iliyopita katika mji wa Chinagodrar.

Waziri wa Ulinzi, Issoufou Katambe alisema taarifa kamili ya idadi ya vifo itatolewa baada ya mkutano wa Baraza la Taifa la Usalama ambao utafanyika leo Jumapili.

Shambulizi la Chinagodrar ambalo limefanyika mwezi mmoja baada ya kikundi kimoja chenye ushirika na kikundi cha kigaidi cha Isis kuua wanajeshi 71, linaashirika kuzorota kwa hali ya usalama katika eneo la Niger linalopakana na nchi za Mali na Burkina Faso.

Mashambulizi yameongezeka mpaka kufikia manne katika kipindi cha mwaka mmoja na kuua karibu watu 400, kwa mujibu wa takwimu za shirika moja la utafiti, licha ya jitihada za vikosi vya kimataifa za kupambana na vikundi vya wapiganaji vyenye ushirika na Isis na Al Qaeda.

Ndege za kijeshi za Ufaransa zilitumika Alhamisi ili kuwatisha washambuliaji, kikosi kazi cha Ufaransa katika kanda hiyo kilieleza, pengine ilisaidia kupunguza madhara zaidi ambayo yangejitokeza.

Hata hivyo, mpaka sasa hakuna kikundi chochote kilichokiri kuhusika katika shambulizi hilo lakini Waziri Katambe alisema kwamba jeshi litaendesha operesheni dhidi ya wapiganaji hao.

Ukanda wa Afrika Magharibi katika jangwa la Sahara limekuwa katika mapigano tangu mwaka 2012 ambapo waasi kutoka kabila la Tuareg walipoungana na kikundi cha waasi na kudhibiti theluthi mbili ya eneo la Mali la Kaskazini, jambo ambalo liliifanya Ufaransa iingilie kati na kuwapiga