Taharuki yatanda Kenya baada ya abiria kusadikiwa kuwa na virusi vya corona

Muktasari:

  • Alikuwa akitokea nchini China na ndege ya Kenya Airways. Wizara ya Afya Kenya imeanza uchunguzi.

Nairobi, Kenya. Abiria mwenye dalili za virusi vya homa ya corona amepelekwa katika Hospitali ya Taifa Kenya baada ya kuwasili katika Uwanja Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA).

Taarifa iliyotolewa na Shirika la Ndege la Kenya (Kenya Airways), imethibitisha kuwa abiria amabaye ni raia wa Kenya aliwasili Nairobi leo Jumanne Januari, 28, 2020 akitokea mjini Guangzhou nchini China.

Shirika hilo limesema kuwa uamuzi wa kumpeleka abiria huyo hospitalini umefikiwa na mamlaka za kituo cha afya cha Serikali kilichopo katika Uwanja wa ndege wa JKIA

Taarifa zinasema kuwa abiria huyo alikaguliwa na mamlaka za afya za viwanja wa ndege nchini China katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Guangzhou kwa ajili ya kurudi nyumbani.

Kwa mujibu wa shirika la ndege la Kenya Airways, abiria wote wanapaswa kupata vipimo katika uwanja wa ndege kabla ya kuingia kwenye ndege

“Wakati abiria wakiwasili kwenye uwanja wa ndege wa JKIA walitakiwa kupata vipimo.”

Katika hatua nyingine, mamlaka za afya nchini Ivory Coast zinaendelea na na uchunguzi wa mwanafunzi anayedaiwa kuwa na virusi vya homa hiyo aliyewasili kutoka Wuhan nchini China.

Mwanafunzi huyo ambaye mamlaka hazikumtaja jina ni wa kwanza kufanyiwa uchunguzi wa virusi hivyo barani la Afrika.

Wizara ya Afya nchini Ivory Coast ilisema kuwa mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 34 aliwasili katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abuja Jumamosi iliyopita akitokea jijini Beijing, China akiwa anakohoa na akipumua kwa shida.

Virusi hivyo vya homa ya corona vimeibuka tangu mwishoni mwa Desemba 2019 na husababisha mafua makali huku dalili zikielezwa kuwa ni mwili kupanda joto.

Mamlaka za China zikisema watu 106 wamepoteza maisha na zaidi ya watu 4,000 wameambukizwa