Uganda yanunua Airbus mbili

Muktasari:

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini Uganda (UCAA), Dk David Kakuba alisema ndege hizo aina ya A330 zitawasili mwaka 2020.

Kampala, Uganda. Serikali ya Uganda imeagiza ndege mbili aina ya Airbus ili kuboresha biashara ya usafiri wa anga nchini humo.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini Uganda (UCAA), Dk David Kakuba alisema “mwaka ujao, Uganda itapata Airbus mbili aina ya A 330.”

Akizungumza wakati wa maadhimisho ya miaka 75 ya Shirika la Kimataifa la Anga (ICAO) yaliyofanyika Jinja kwenye chanzo cha Mto Nile, Mkurugenzi huyo alisema ndege hizo zinatarajia kufanya safari zake katika nchi za Uingereza, India na China.

“Ninatoa wito kwa Waganda kuunga mkono shirika ya ndege letu badala ya kulizungumzia  vibaya. Tunapaswa kujivunia vya kwetu kwasababu zitaongeza utalii na hatimaye nchi kujipatia kuongeza pato la Taifa.”

Awali waziri wa Kazi na uchukuzi, Monica Azuba alisema ndege hizo zinatarajiwa kuwasili mwaka 2020 na kuongeza kuwa kwa sasa shirika lina ndege zaidi ya 10.

Alisema ndege hizo zitaleta ushindani mkubwa kwa safari za kimataifa. “Ujaji wa ndege hizi utasaidia ushindani wa kibiashara wa ndani na nje ya nchi na kukuza utalii wetu kwani sasa wataweza kuja moja kwa moja,” alisisitiza.