Waziri mkuu Ukraine ajiuzulu kwa kumtukana rais

Muktasari:

Amerekodiwa akimtukana rais wa nchi hiyo, Volodymyr Zelensky

Waziri mkuu wa Ukraine amewasilisha barua yake ya kujizulu kwa Rais Volodymyr Zelensky, kufuatia ripoti za kurekodiwa akitoa matamshi ya matusi dhidi ya rais huyo.

Oleksiy Honcharuk (35) amesema hatua yake ya kujiuzulu imenuia kuondoa shaka juu ya heshima na utiifu alionao kwa rais.

Vyombo vya habari vya Ukraine viliripoti juu ya sauti iliyorekodiwa ambamo Honcharuk anadaiwa kumuelezea Zelensky kama mtu mwenye ufahamu wa kale kuhusu masuala ya kiuchumi na uwezo mdogo wa kujifunza kuhusu nyanja hiyo.

Haikubainika wazi iwapo Honcharuk, mwanasheria aliyeunga mkono mageuzi makubwa ya kiuchumi, ataacha kweli nafasi hiyo. Bunge litapaswa kuidhinisha barua yake ya kujiuzulu.

Haikufahamika mara moja iwapo Rais huyo atakubali barua hiyo.

Zelensky, msanii wa vichekesho ambaye hakuwa na uzoefu wowote kisiasa, aliingia madarakani baada ya kupata ushindi mkubwa mwaka jana na chama chake cha Mtumishi wa watu kilipata wabunge wengi na kuunda serikali.