Halmashauri Sengerema yawapa wamachinga maeneo ya kufanyia biashara

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Sengerema Magesa Mafuru akizungumuza na wamachinga mara baada ya kuwagawia maeneo ya kujenga vibanda ndani ya soko kuu mjini Sengerema leo. Picha na Daniel Makaka.

Muktasari:

Halmashauri ya Sengerema Mkoa wa Mwanza imewagawia maeneo wafanyabiashara wadogo 307 kati soko kuu la Wilaya hiyo.

Sengerema. Halmashauri ya Sengerema Mkoa wa Mwanza imewagawia maeneo wafanyabiashara wadogo 307 kati soko kuu la Wilaya hiyo.

Ugawaji huo wa maeneo umefanyika leo Ijumaa Novemba 29, 2019 na mkurugenzi wa halmashauri ya Sengerema, Magesa Mafuru aliyewataka wamachinga kutumia fursa hiyo kuendesha maisha yao.

“Halmashauri tumeamua kuwagawia maeneo wamachinga katika soko ili wafanye biashara katika maeneo mazuri na kuondoka kwenye barabara,” amesema Mafuru.

Amebainisha kuwa ugawaji huo umezingatia jinsia, hakuna malalamiko yoyote.

Mwenyekiti wa wafanyabiashara wadogo wilayani Sengerema, Maneno Juma amesema licha ya ugawaji huo kufanyika, wafanyabiashara wadogo 100 wamekosa maeneo na kuziomba mamlaka husika kuwapatia maeneo.

Mmoja wa wafanyabiashara hao, Vedastus Zeba ameishukuru Serikali kwa kuwapatia maeneo hayo.