Hospitali ya Muhimbili yabainisha mkakati wa kunusuru vifo vya wajawazito

Muktasari:

Hospitali ya Taifa Muhimbili yaanzisha chumba cha uangalizi maalum (ICU) ndani ya jengo la wazazi kwa ajili ya kunusuru maisha ya wanawake wanaokutana na changamoto wakati wa kujifungua

Dar es Salaam. Katika kukabiliana na vifo vya wajawazito Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) nchini Tanzania imetengeneza chumba cha uangalizi maalum ndani ya wodi ya wazazi.

Chumba hicho mahususi cha  huduma ya uangalizi maalumu (MAICU) kina vitanda 10, mashine tano za kusaidia kupumua na ultrasound.

Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya kina mama na uzazi, Dk Vicent Tarimo akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Juni 25, 2019 amesema uwepo wa  chumba hicho unasaidia kuokoa maisha ya wanawake wanaokutana na changamoto wakati wa kujifungua.

Amesema awali wastani wa vifo 120 vinavyotokana na uzazi vilikuwa vikitokea kwa mwaka lakini tangu chumba hicho kianze kufanya kazi vifo vimepungua.

“Vifo vingi vya wanawake vinatokana na kifafa cha mimba na kupoteza damu, sasa uwepo wa chumba hiki unarahisisha utoaji wa huduma za dharura kuokoa maisha,” amesema

“Awali ilikuwa inalazimu kwenda umbali wa mita 150 kutoka jengo la wazazi kwenda kufuata ICU, sasa hivi uangalizi maalum unafanyika ndani ya wodi,” amesema

Katika hatua nyingine, hospitali hiyo imefanya ukarabati wa wodi tatu hadi sita za Mwaisela na kuweka mfumo wa oxygen pamoja na vitanda saba  kila wodi sawa na vitanda 28 vya kutoa huduma kwa wagonjwa maalumu.