Kigogo amkingia kifua kocha Spurs

Muktasari:

Kocha wa Tottenham Hotspurs, Mauricio Pochettino amesema licha ya kuboronga katika mashindano ya msimu huu, kibarua chake kinalindwa na mwenyekiti wake Daniel Levy.  


London, England. Licha ya kufungwa mabao kumi ndani ya wiki moja, kocha Mauricio Pochettino, amesisitiza kibarua chake kipo salama.

Pochettino alisema licha ya kupata matokeo mabaya analindwa na bosi wake Daniel Levy.

Spurs ilicharazwa na Bayern Munich ya Ujerumani mabao 7-2 kabla ya kulala 3-0 ilipovaana na Brighton.

Pochettino alisema licha ya kupata matokeo mabaya msimu huu bado ana uhusiano mzuri na mwenyekiti wa klabu hiyo.

“Tuna uhusiano mzuri sana na ananiunga mkono kwa nguvu zote. Siku zote nimekuwa nikisema ingawa ni mwenyekiti, lakini ni rafiki yangu,” alisema Pochettino.

Nyota huyo wa zamani wa Argentina alidai mpira si maigizo ni mchezo wa furaha ambao hauwezi kuwatenganisha kutokana na mihemko ya baadhi ya watu.

Hata hivyo, Pochettino alisema amejifunza kupitia matokeo mabaya iliyopata Spurs na mkakati wake ni kuirejesha katika mstari wa kuwania ubingwa msimu huu.

Pia alisema watu waliokasirishwa na matokeo mabaya wana haki ya kufanya hivyo kwa kuwa kila mmoja alikuwa na matumaini ya Spurs kupata matokeo mazuri.

“Katika miaka yangu mitano na nusu, siku tano za mwisho zilikuwa ngumu sana kwangu, katika soka kufungwa mabao 7-2 na 3-0,” alisema Pochettino.