Kutosajili laini ya simu faini Sh5 milioni, jela miezi 12-Muswada

Dodoma. Ni nadra kwa Bunge kumaliza mkutano mmoja bila ya kufanya marekebisho ya sheria, na Bunge linaloanza vikao vyake leo, litayafanyia marekebisho sheria kadhaa, ikiwemo itakayompeleka gerezani kwa miezi 12 au kulipa faini ya Sh5 milioni, mtumiaji wa laini ya simu isiyosajiliwa.

Hii itawezekana kama Bunge la Jamhuri ya Muungano litakubaliana na mapendekezo ya Serikali ya kurekebisha Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta, ikiwa ni moja ya mapendekezo ya mabadiliko kadhaa yatakayowasilishwa katika mkutano huo wa 16.

Katika marekebisho hayo, Serikali pia inapendekeza adhabu kwa mtoa huduma, msambazaji, wakala ama aliyethibitishwa kushughulika na uuzaji ama usambazaji wa kadi za simu za mkononi, atakayesababisha kwa namna yoyote kutumika kwa laini ya simu isiyosajiliwa.

Kwa kundi hilo, mapendekezo yanataka wahusika watozwe faini isiyopungua Sh10 milioni au kifungo kisichopungua miaka miwili jela au vyote kwa pamoja.

Serikali iliamua kuachana na usajili wa zamani wa laini baada ya kuona mfumo uliokuwepo unatumiwa vibaya na wahalifu ambao waliweza kusajili chipu za simu kwa kutumia picha ya mtu yeyote.

Kwa undani wa Habari hii pata nakala ya Gazeti la Mwananchi Jumanne 3, Septemba, 2019.