Ndairagije kocha wa muda Stars

Muktasari:

 Ndayiragije amefanya kazi nchini Tanzania kwa miaka mitatu sasa tangu mwaka 2016 alipojiunga na Mbao FC na baadaye alitimkia KMC ambayo aliinoa msimu uliopita kisha kuelekea Azam FC anayoitumikia kwa sasa

Kocha Mkuu wa Azam FC, Etienne Ndayiragije ameteuliwa kuwa Kocha Mkuu wa muda wa timu ya taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' kushika nafasi ya Emmanuel Amunike aliyetimuliwa.

 

Uteuzi wa Ndayiragije ambaye kwa sasa yuko nchini Rwanda akiiongoza Azam FC kwenye mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup) umetangazwa leo mara baada ya kamati ya utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kukutana kwa dharura jijini Dar es Salaam leo.

 

"Kikao hicho ambacho kipo kwa mujibu wa Katiba ya TFF Ibara ya 40 (110 kilifikia maamuzi hayo baada ya kujiridhisha na uwezo wa kocha huyo na mafanikio aliyoyapata, akifundisha timu mbakimbali za Tanzania ambazo ni Mbao na KMC. Ambapo Etienne akiwa na KMC katika msimu wake wa kwanza alifanikiwa kukiwezesha kikosi hicho kupata nafasi ya kucheza Kombe la Shirikisho la CAF pamoja na kutinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la FA.

 

Etienne ambaye atakiongoza kikosi hicho katika michezo ya kuwania kufuzu mashindano ya CHAN, amependekeza benchi lake la ufundi kusaidiwa na kocha wa Coastal Union, Juma Mgunda pamoja na kocha msaidizi wa Pokisi Tanzania, Seleman Matolab ambao uteuzi huo umezingatia programu maalum ya kuendeleza makocha wazawa.

 

Kwa upande wa meneja wa kikosi, atakuwa Nadir Haroub 'Cannavaro' huku kocha wa makipa akiwa ni Saleh Ahmed Machupa ambaye anafundisha Malindi ya Zanzibar," ilisema taarifa hiyo ya TFF.

 

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ndayiragije atatangaza kikosi chake, keshokutwa Jumamosi.