Ndege ya Air Tanzania yazuiwa kuondoka Afrika Kusini kwa amri ya mahakama

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imewaomba radhi abiria waliokuwa katika ndege ya  Air Tanzania iliyozuiwa kuondoka Afrika Kusini kwa amri ya mahakama

Dar es Salaam. Ndege ya Air Tanzania iliyokuwa inatoka Afrika Kusini kwenda jijini Dar es Salaam, Tanzania imezuiwa kuruka kwa amri ya Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg nchini humo.
Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa   Agosti 23, 2019 na katibu mkuu Wizara ya Ujenzi,  Uchukuzi na Mawasiliano, Dk Leonard Chamuriho inaeleza kuwa Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya mwanasheria mkuu inafuatilia suala hilo ili ndege hiyo iachiwe na kuendelea na safari zake kama kawaida.
"Waziri wa Ujenzi,  Uchukuzi na Mawasiliano anaomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza kwa abiria wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) waliokuwa wanasafiri leo kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Oliver Tambo,  Johannesburg kuja Dar es Salaam kufuatia ndege hiyo kushindwa kufanya safari kama ilivyopangwa, " inaeleza taarifa hiyo.
Inabainisha kuwa kwa mujibu wa taarifa ambazo Serikali imepokea kutoka kwa balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, ndege hiyo imezuiwa kwa amri ya mahakama hiyo.