VIDEO: Kikwete asema nguvu ya kupambana na malaria imeshuka

Kikwete asema nguvu ya kupambana na malaria imeshuka

Muktasari:

Mjumbe wa baraza la kupambana na malaria duniani, Rais mstaafu Jakaya Kikwete amesema nchi za Afrika zinatakiwa kuwekeza katika uongozi, fedha na teknolojia ili ziweze kutokomeza ugonjwa wa malaria.

Dar es Salaam. Mjumbe wa baraza la kupambana na malaria duniani, Rais mstaafu Jakaya Kikwete amesema nchi za Afrika zinatakiwa kuwekeza katika uongozi, fedha na teknolojia ili ziweze kutokomeza ugonjwa wa malaria.

Baraza hilo linaundwa na jopo la watu mashuhuri 11 duniani waliojitolea kupambana na malaria akiwemo mwenyekiti wa baraza hilo Bill Gates, Aliko Dangote, Peter Chenin, mfalme wa Eswatini, Graca Macheli na wengineo.

Kikwete ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Novemba 7, 2019 wakati akizungumza katika kikao cha baraza la mawaziri wanaoshughulikia sekta ya afya na Ukimwi kutoka nchi za Jumuiya ya Maendeleo  Kusini mwa Afrika (Sadc).

“Sisi tumedhamiria kuiondoa kabisa malaria kwenye sura ya dunia, tunachokifanya sasa ni kuhakikisha tunazungumza na watunga sera ndio maana nimekuja kuongea na mawaziri hawa.”

 

“Kwa nchi za Sadc, malaria itakwisha kabisa ikiwa zitaongeza fedha kwa ajili ya kugharamia, kikubwa hasa ni kuwa na uongozi, fedha na kuwekeza katika teknolojia,” amesema Kikwete.

 

Amesema katika nchi za Sadc kuna baadhi ya malengo zimefikia, mengine hawajatimiza ikiwemo kutumia dawa mseto.

Amesema nguvu kubwa ya kupambana na ugonjwa huo imeshuka ikilinganishwa na mwaka 2000 mpaka 2015 na tangu wakati huo duniani kote kasi ya kupambana na ugonjwa huo imeshuka.

Amesema licha ya hivyo ugonjwa huo kupunguzwa  na vitu vitatu ikiwemo kutumia dawa mseto, chandarua kilichowekwa dawa na kupaka dawa kwenye ukuta.

“Hayo ndiyo mambo tufanye sasa,  nchi za Sadc zimekubaliana kufikia asilimia 80 ya matumizi ya chandarua lakini baadhi ya nchi hazijafikiwa,” amesema Kikwete.