Mbowe, Nyalandu walivyoingia maadhimisho miaka 58 ya Uhuru

Muktasari:

Suala la kunyimwa fursa ya kufanya mikutano ya kisiasa, viongozi na wanachama wake kukamatwa, kushikiliwa na kufikishwa mahakamani wakiwa katika shughuli za kisiasa ni kati ya hoja zilizotumiwa na Chadema na vyama vingine vya upinzani kususia kushiriki shughuli kadhaa za Kitaifa.

Mwanza. Wameshiriki kweli aise! Hiyo ni kati ya kauli zinazoweza kuwa zimetolewa na watu baada ya kumwona Mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania cha Chadema, Freeman Mbowe akiingia ndani ya uwanja wa CCK Kirumba jijini Mwanza kuhudhuria maadhimisho ya Kitaifa ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika.
Hata hivyo, Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Kati, Lazaro Nyalandu hawakuvaa sare maalum za chama wala kombati ambazo zinatumiwa kama vazi maalum chama chao lakini wamepigilia suti nyeusi, mashati meupe na tai.
Uwanjani pia hawajaonekana wananchi waliovaa sare wala vazi linaloonekana kama alama ya Chadema tofauti na wenzao wa CCM ambao baadhi yao wamevaa sare rasmi za chama za rangi ya kijani na njano.
Akiwa ameongozana na Nyalandu aliyewahi kuwa waziri wa maliasili na utalii wa Tanzania, Mbowe ameingia uwanjani kupitia lango la viongozi wa kitaifa na kupokelewa kwa heshima zote kama ilivyofanyika kwa viongozi wengine.
Baada ya kupokelewa, Mbowe na Nyalandu wameongozwa moja kwa moja na kuonyeshwa eneo la kuketi katika jukwaa kuu waliko viongozi wengine wa kitaifa wa sasa na wastaafu.
Kushiriki kwa Mbowe kwenye maadhimisho ya mwaka huu kumehitimisha ‘mgomo’ wa karibia miaka minne tangu mwaka 2015 wa Chadema na viongozi wake kususia kushiriki maadhimisho ya kitaifa.
Mkurugenzi wa Mambo ya Nje, Itikadi na Uhusiano wa Umma wa Chadema, John Mrema aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana Jumapili Desemba 8, 2019 kuwa chama hicho kimetafakari na kuamua kushiriki maadhimisho ya mwaka huu kwa sababu kinajiandaa kushika Dola.
“Ni kweli tangu Serikali ya awamu ya tano iingie madarakani hatujawahi kushiriki sherehe za Uhuru. Tumezingatia mambo mbalimbali miongoni ni kwamba sisi ni chama kinachojiandaa kushika Dola na kwa sababu za nyakati na muda ambao tupo, tumeamua kushiriki,” alikaririwa Mrema
“Kwa miaka mitatu tumekuwa tukishauriana ndani ya chama, nje ya chama na wadau mbalimbali. Kama chama tumefanya uamuzi wetu tunaamini ni sahihi na baadaye tutawaeleza wanachama wetu kwa kina na mapana,” aliongeza