Maalim Seif, mwenzake waitwa Polisi Pemba

Muktasari:

Aliyewahi kuwa Makamu wa kwanza wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amepewa wito wa kufika kituo cha polisi wilaya ya Wete Pemba visiwani Zanzibar.

Unguja. Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba visiwani Zanzibar limemtaka Mshauri mkuu wa Chama cha ACT- Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad kufika kituo cha Polisi Wilaya ya Wete kesho Jumanne Januri 14, 2020 saa tatu asubuhi.

Mbali na Maalim Seif, mwingine ni Mwenyekiti wa Kamati ya Itikadi, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa chama hicho, Salim Bimani.

Mwananchi limezungumza na Bimani ambaye amekiri kupokea wito wa kuwataka kufika kituo hicho cha polisi.

“Tutaondoka kesho asubuhi mapema sana kuelekea Pemba na mara baada ya kufika tutakwenda moja kwa moja tulipoitwa,” amesema Bimani.

Hata hivyo, Mwananchi limemtafuta kamanda wa mkoa wa kaskazini Pemba kupitia simu zake za mkononi bila mafanikio kwani inaita bila kupokelewa.

Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mohamed Haji Hassan amesema ana taarifa za wito huo lakini hakutaka kuongea zaidi kwani hana taarifa za kutosha juu ya wito huo.