Kuanzia Mwezi wa Ramadhani biashara soko la Kariakoo kufanyika saa 24

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kuanzia Mwezi wa Ramadhani  mwaka 2020 biashara katika soko la Kariakoo jijini Dar es Salaam zitafanyika saa 24.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema kuanzia Mwezi wa Ramadhani  mwaka 2020 biashara katika soko la Kariakoo jijini Dar es Salaam zitafanyika saa 24.

Amesema kipindi hicho ndio utafanyika uzinduzi, kuanzia hapo biashara itaendelea kutolewa saa 24.

Ameeleza hayo leo Jumanne Februari 25, 2020 katika kikao cha kamati ya ushauri ya Mkoa wa Dar es Salaam, kuwataka wafanyabiashara kujiandaa kujihakikishia ulinzi wa kutosha ili wakati utakapofika, wafanye biashara zao bila wasiwasi.

“Kariakoo ya usiku na mchana itafungua fursa mpya za uchumi Dar es Salaam, napendekeza mpango huu uanze rasmi wakati wa mwezi wa Ramadhani ili ndugu zetu waanze kuhudumiwa masaa 24.”

“Mkoa wetu lazima uendelee kuwa kitovu cha biashara na naendelea kusisitiza tu ufungaji wa Kamera za ulinzi,” amesema Makonda.