90,104 kufanya mtihani darasa la nne, kidato cha pili Zanzibar

Waziri wa elimu na mafunzo ya amali Zanzibar Riziki Pembe Juma akitoa taarifa mbele ya waandishi wa habari.Picha na Muhammed Khamis

Muktasari:

  • Waziri wa elimu na mafunzo ya Amali Zanzibar,  Riziki Pembe Juma  amesema wanafunzi 55,635 watafanya mtihani wa darasa la nne.

Unguja. Waziri wa elimu na mafunzo ya Amali Zanzibar,  Riziki Pembe Juma  amesema wanafunzi 55,635 watafanya mtihani wa darasa la nne.

Amesema kati ya wanafunzi hao watakaofanya mtihani huo Novemba 25, 2019, wavulana ni 28,256 na wasichana 27,379 sawa na ongezeko la asilimia 16 ikilinganishwa na  mwaka 2018.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Novemba 22, 2019 mjini Unguja katika mkutano wake na waandishi wa habari.

Amesema watahiniwa 34,469 wameandikishwa kufanya mtihani wa kuingia kidato  cha tatu, “wasichana ni 18,502 na wavulana ni 15,967 sawa na upungufu wa asilimia moja  ikilinganishwa na idadi ya watahiniwa waliosajiliwa kufanya mtihani huu mwaka 2018.”

Amewataka wazazi na walezi kuwa karibu zaidi na watoto wao wanaofanya mitihani kuhakikisha wanafika katika vituo vyao vya mitihani kwa wakati na kuwataka watahiniwa kujiepusha na udanganyifu.