VIDEO: ACT Wazalendo yamtumia ujumbe Waziri Jafo, yataka tume huru ya uchaguzi

Muktasari:

  • ACT Wazalendo wasisitiza kutoshiriki uchaguzi serikali za mitaa watoa msimamo ikiwamo wasimamizi wa uchaguzi huo wawajibishwe.

Dar es Salaam. Chama cha ACT Wazalendo kimeendelea kutoa msimamo wa kutoshiriki uchaguzi wa serikali za mitaa Novemba 24, 2019.

Msimamo huo umetolewa ikiwa ni siku moja baada ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo kuwarejesha wagombea wote waliochukua na kurejesha fomu za uchaguzi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Novemba 11, 2O19 Mwenyekiti wa kampeni na uchaguzi wa chama hicho, Joran Bashange amesema hawatashiriki uchaguzi hadi mapendekezo yao yatakapokubaliwa na kufanyiwa kazi.

"Tunaendelea kusisitiza msimamo wetu wa kujitoa kwenye uchaguzi na kuwataka wanachama wetu wote nchi nzima kuendelea kutekeleza agizo la chama  lakuandika barua za kujitoa kwenye uchaguzi" amesema Bashange

Amesema uamuzi huo wa yalifanywa na kikao halali cha chama na hayawezi kutenguliwa na kauli za Waziri.

"Wakati wa uchukuaji na urejeshaji fomu  wasimamizi wasaidizi walionekana kufanya kazi kinyume na kanuni na miongozo ikiwemo kufunga ofisi, kukataa kutoa fomu na maeneo mengine wasimamizi kutokuwa na fomu," amesema

"Baada ya mambo haya kutokea tulimwandikia Waziri mwenye dhamana barua kumtaka aingilie kati lakini hakuna hatua iliyochukuliwa na kusababisha maeneo hayo kukosa wagombea," amesema

Amesema Waziri Jafo anapotangaza wananchi wote waliojaza fomu kuruhusiwa kugombea na  mchakato wa uchaguzi kuendelea wapo waliokoseshwa haki kwa kunyimwa fomu.

Bashange amesema msimamo wa chama kuhusu uchaguzi  ni pamoja na mchakato mzima kuanza upya na kufuta yote yaliyofanywa chini ya utaratibu wa sasa.

Amesema jambo lingine ni kutunga kanuni mpya za uchaguzi kwa makubaliano na maridhiano ya vyama vya siasa na kuundwa kamati huru ya kusimamia uchaguzi.

Aidha Bashange amesema chama hicho kinamtaka Waziri Jafo kuitisha kikao cha pamoja cha vyama vyote vya siasa ili kukubaliana namna ya kusonga mbele na kuviita vyama hivyo kutumia nafasi hiyo kwa pamoja kudai tume huru ya uchaguzi.

Bashange amesema wasimamizi wa uchaguzi wote walioharibu mchakato wa uchaguzi huu wawajibishwe ili kukomesha tabia hii inayoharisha amani ya nchi.

“Tunatoa wito kwa vyama vyote vya siasa kutokubali hadaa ya Waziri Jafo na kutumia nafasi hii kuwa pamoja kudai Tume Huru ya Uchaguzi ili Uchaguzi wa mwaka 2020 usiwe na dosari tulizoshuhudia sasa. Bila Tume Huru ya Uchaguzi pasiwe na Uchaguzi wowote nchini. Viongozi wa Kitaifa wa vyama watoke na tamko la pamoja kutaka Tume Huru ya Uchaguzi,” amesema Bashange