ATCL yaokoa Sh590 milioni matengenezo ya Bombardier

Muktasari:

Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) limesema kwa sasa linafanya matengenzo makubwa na madogo nchini Tanzania na kupunguza gharama zilizokuwa zikitumika kuzifanyia matengezo nje ya nchi hiyo.

Mwanza. Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) limeendelea kujiimarisha kiutendaji ikiwamo kujenga uwezo wa matengenezo madogo na makubwa ya ndege zake aina ya Bombardier Q-400.

Kwa uwezo huo, ATCL imeokoa gharama ya Dola 260 za Kimarekani sawa na Sh590 milioni ambazo zingetumika kutengeneza ndege hizo nje ya Tanzania.

Akitoa taarifa ya utekelezaji kwa Rais wa Tanzania, John Magufuli wakati wa hafla ya kupokea ndege mpya ya Bombardier Q-400 katika uwanja wa ndege wa Mwanza leo Desemba 14, 2019, Mkurugenzi Mkuu wa ATCL, Ladislaus Matindi amesema shirika hilo linaendelea kutekeleza mikakati ya kuwa na uwezo wa kufanyia matengenezo madogo na makubwa ndege zake kubwa.

“Hivi sasa tunaweza kuunda na kutengeneza matairi ya ndege zote za ATCL. Uwezo huo umepunguza gharama zilizokuwa zikitumika kuunda na kutengeneza matairi katika nchi za Kenya na Ethiopia,” amesema Matindi

Amesema matengenezo hayo yanayofanyika katika karakana ya ATCL iliyoko jijini Dar es Salaam pia umepunguza muda wa kuunda na kutengeneza matairi hayo nje ya Tanzania.