Adaiwa kumuua mkewe kwa wivu wa mapenzi, alimchoma mkuki akiwa usingizini

Muktasari:

Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora nchini Tanzania wanamshikilia  mkazi wa kijiji cha Isikizya, Omary Dweka maarufu  Mkuyu kwa tuhuma za kumuua mkewe, Hawa Juma kwa kumchoma mkuki.

Tabora. Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora nchini Tanzania wanamshikilia  mkazi wa kijiji cha Isikizya, Omary Dweka maarufu  Mkuyu kwa tuhuma za kumuua mkewe, Hawa Juma kwa kumchoma mkuki.

Akizungumza leo Jumanne Februari 25, 2020 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Barnabas Mwakalukwa amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo katika kijiji hicho kilichopo barabara kuu ya kuelekea Wilaya ya Nzega.

Amebainisha kuwa alimchoma mkuki mgongoni na kutokea kifuani upande wa kushoto, alifanya kitendo hicho wakati mkewe amelala.

“Mtuhumiwa amekamatwa na atafikishwa mahakamani muda wowote kwani upelelezi umekamilika,” amesema Kamanda Mwakalukwa akibainisha chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa mapenzi.

Amesema wivu wa mapenzi, kugombania mali husababisha familia kusambaratika, “kama huyu mwanaume, sasa anakabiliwa na kesi na kuiacha familia haina mwangalizi na akifungwa familia inabaki inateseka.”