VIDEO: Agizo la Magufuli latekelezwa, bibi wa miaka 80 arejeshewa nyumba

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo

Muktasari:

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo ametekeleza agizo la Rais wa Tanzania,  John Magufuli kumrudishia nyumba bibi mwenye umri wa miaka 80, Amina Muhenga aliyoidai zaidi ya miaka 30.

Dar es Salaam. Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo ametekeleza agizo la Rais wa Tanzania,  John Magufuli kumrudishia nyumba bibi mwenye umri wa miaka 80, Amina Muhenga aliyoidai zaidi ya miaka 30.

Rais Magufuli alitoa agizo hilo miezi miwili iliyopita alipokuwa katika ibada ya Jumapili Kanisa la mtakatifu Petro, jijini Dar es Salaam.

Bibi huyo alimfuata kiongozi mkuu huyo wa nchi na kumueleza malalamiko yake kuhusu nyumba yake kuchukuliwa na mtu mwingine kinyume na taratibu, kumsababishia kukosa makazi maalumu ya kuishi.

Leo Jumamosi Novemba 9, 2019, Chongolo ameeleza kuwa baada ya Rais kutoa maagizo hayo, walichukua jukumu la kumrudishia Amina nyumba yake pamoja na hati huku utaratibu mwingine ukiendelea kufanyika.

“Baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa Amina Rais alituagiza kulifanyia kazi na leo hii tumehitimisha kwa kumkabidhi hati za umiliki wa nyumba yake, na mambo mengine tunaendelea kuyakamilisha. Kuanzia sasa bibi anarudi kwenye nyumba yake,” amesema Chongolo.