Ambaka mtoto wa darasa la sita hadi kumuua

Muktasari:

  • Mponjoli Lisa, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa madai ya kumbaka binti wa darasa la sita Shule ya Msingi Pugu Kajiungeni hadi kumuua.

Dar es Salaam. Mponjoli Lisa, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa madai ya kumbaka binti wa darasa la sita Shule ya Msingi Pugu Kajiungeni hadi kumuua.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne Desemba 10, 2019 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala, Zuberi Chembela amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba watu wanne wanashikiliwa na polisi.

Mwenyekiti wa mtaa wa Pugu Bombani, Amanzi Bungara amesema tukio hilo limetokea Jumapili Desemba 8, 2019 na kudai kuwa Lisa baada ya kufanya tukio hilo alijisalimisha kituo cha polisi Stakishari na kukiri kufanya kitendo hicho.

“Lisa alikwenda nyumbani kwa huyo binti na kuomba amsindikize dukani na walipokuwa njiani alimfanyia kumfanyia unyama huo. Tumemzika leo jioni katika makaburi ya Mwakanga.”

“Kutokana na tukio hili limewaagiza wakazi wa mtaa wangu kuorodhesha majina ya wapangaji wao ili niwajue, lakini tumepanga kuanzisha ulinzi shirikishi,” amesema Bungara.

Mwenyekiti huyo wa mtaa amesema mtuhumiwa huyo alijisalimisha polisi na kukiri kufanya kitendo hicho.

Kamanda Chembela ameahidi kutoa ufafanuzi wa tukio hilo kwa kina kesho Jumatano Desemba 11, 2019.