Askofu Bagonza ataja makomandoo saba mapambano rushwa, ufisadi

Muktasari:

  • Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT), Dayosisi ya Karagwe mkoani Kagera, Dk Benson Bagonza amesema vita dhidi ya ufisadi, rushwa na wizi wa rasilimali za Taifa haiwezi kufanikiwa bila kushirikisha kile alichokiita makomandoo saba wazoefu

Arusha. Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT), Dayosisi ya Karagwe mkoani Kagera, Dk Benson Bagonza amesema vita dhidi ya ufisadi, rushwa na wizi wa rasilimali za Taifa haiwezi kufanikiwa bila kushirikisha kile alichokiita makomandoo saba wazoefu.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Mei 24, 2019 jijini Arusha katika kongamano la vijana kuhusu matumizi chanya ya mitandao ya kijamii.

Amewataja makomandoo hao kuwa ni; mitandao ya kijamii,  vyombo huru vya habari, asasi za kiraia na taasisi zisizo za Serikali, vyama vya wafanyakazi, vyama vya upinzani, Bunge huru na Katiba nzuri.

 “Kuwapunguzia uhuru makomandoo hawa au kugombana nao badala ya kugombana na ufisadi ni kutangaza kushindwa kabla ya mapambano kuanza,” amesema.

Amebainisha  kuwa matumizi chanya ya mitandao ya kijamii ni nyenzo nzuri ya utetezi katika jamii lakini wasioliona hilo ni wale wanaodhani kwa nafasi zao, hawahitaji kutetewa.

Askofu Bagonza katika mambo hayo saba, amechambua jinsi yanavyoweza kutumika katika mapambano ya rushwa na ufisadi na hatimaye Taifa liondokane na mambo hayo.

“Mitandao ya kijamii ina nguvu ya udhibiti wa matumizi mabaya ya madaraka na dhambi nyingine  katika jamii.”

“Taifa letu chini ya serikali  ya Awamu ya Tano limetangaza vita kali dhidi ya ufisadi, rushwa na wizi wa raslimali za taifa. Ili kushinda vita hii, Serikali inahitaji msaada wa makomandoo wazoefu katika vita ya namna hii.”