Askofu Ruwaichi afanyiwa upasuaji MOI

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam nchini Tanzania, Mhashamu Yuda Thadeus Ruwa'ichi

Muktasari:

Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) imesema ilimpokea Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mhashamu Yuda Thadeus Ruwa'ichi kutoka Hospitali ya KCMC na kumfanyia vipimo jana usiku, kabla ya kumfanyia upasuaji uliochukua saa tatu.

Dar es Salaam. Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam nchini Tanzania, Mhashamu Yuda Thadeus Ruwa'ichi amefanyiwa upasuaji wa dharura katika Taasisi ya mifupa (MOI).

Taarifa iliyotolewa na leo Jumanne Septemba 10, 2019 na Kitengo cha Mawasiliamo MOI inaeleza Askofu Ruwa'ichi alipokelewa hospitalini hapo jana Jumatatu saa 5 usiku akitokea Hospitali ya KCMC, Moshi mkoani Kilimanjaro.

Baada ya kupokelewa hospitalini hapo, wataalamu wa MOI walimfanyia uchunguzi na vipimo na kubaini alihitaji upasuaji wa dharura.

“Jopo la madaktari bingwa pamoja na wauguzi wa taasisi ya MOIi walimfanyia upasuaji mkubwa kwa muda wa saa 3 kuanzia saa 7 usiku hadi saa 10 alfajiri na upasuaji huo ulifanyika kwa mafanikio makubwa,” imeeleza taarifa hiyo

“Baada ya upasuaji huo hali ya Askofu Ruwa'ichi inaendelea vizuri na bado yuko katika chumba cha uangalizi maalumu (ICU).”

Taarifa hiyo imesema tunawatoa hofu Watanzania hususani wa Kanisa Katoliki wazidi kumuombea ili aweze kupona mapema na kurejea kwenye majukumu yake.