Azamisha mtoni gari alilopewa zawadi

Muktasari:

Ni baada ya kuchukizwa na zawadi ya gari aina ya BMW aliyopewa katika siku yake ya kuzaliwa badala ya Jaguar.

India.  Ukistajabu ya Mussa utayaona ya firauni, raia mmoja nchini India amewaacha midomo wazi ndugu, jamaa na marafiki zake baada ya kulitumbukiza mtoni gari aina ya BMW aliyopewa zawadi.

Shirika la habari la BBC, lilieleza kuwa mwanaume huyo alifikia hatua hiyo baada ya kukasilishwa na zawadi hiyo ambayo alipewa na familia yake katika hafla ya kusherehekea siku yake ya kuzaliwa

Kwa mujibu wa BBC, mwanaume huyo alikasirishwa na kitendo cha kununuliwa BMW badala ya gari aina ya Jaguar.

Inaelezwa kuwa mwanaume huyo ni mtoto wa tajiri mkubwa nchini humo anayemiliki biashara kadhaa ikiwamo majumba makubwa ya kifahari.

Kipande cha video kilichosambaa katika mitandao ya kijamii kilimuonyesha mwanaume huyo akiikokota BMW hiyo katika  mto mkubwa uliopo katika Jimbo la Haryana, Kaskazini mwa India.

Polisi nchini India imedhibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba inaendelea na uchunguzi wa kisa hicho.